Wabunge wahojiwa kuchochea kilimo cha bangi - KATUMA BLOG tz.

HABARI ZA HIVI PUNDE

KWA HABARI ZA UHAKIKA NA KUAMINIKA


Post Top Ad

Responsive Ads Here

Tuesday, August 8, 2017

Wabunge wahojiwa kuchochea kilimo cha bangi



Related image

WABUNGE wawili wa Tarime Vijijini, John Heche na wa Tarime Mjini, Esther Matiko wote kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), wamejikuta mikononi mwa Polisi kwa tuhuma mbili tofauti.

Tuhuma hizo ni kudaiwa kuchochea wananchi kulima zao haramu la bangi vile vile kuwachochea wananchi kuvamia mgodi wa Acacia North Mara.

Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Tarime/Rorya, Henry Mwaibambe amethibitisha kuwa Polisi imewakamata wabunge hao kwa uchochezi na kwamba wanawahoji.

Kamanda Mwaibambe alisema Heche na Matiko wote wana makosa mawili kila mmoja; kuwachochea wananchi kulima zao haramu la bangi na tuhuma ya pili ni kuwachochea wananchi kuvamia mgodi wa Acacia North Mara.

Alisema Heche anadaiwa kuchochea wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika Sirari, kulima bangi na kosa lingine kuwachochea wananchi kuvamia mgodi wa Acacia North Mara uliopo Nyamongo na kusababisha hasara ikiwemo kuharibu mali na kujeruhi walinzi wakiwemo askari Polisi

“Matiko anatuhumiwa kwenda Jimbo la Tarime Vijijini katika mkutano wa Heche huko Sirari na kuwachochea wananchi kulima bangi badala ya kulima miwa. Watuhumiwa wanahojiwa na hatua zaidi zitachukuliwa dhidi yao,” alisema Kamanda Mwaibambe.

Wabunge hao walipohojiwa wakiwa katika Kituo cha Polisi Tarime, walikiri kushikiliwa na kuhojiwa kwa tuhuma hizo, lakini walikana kufanya uchochezi.

“Mimi juzi (Jumamosi) niliambiwa kuwa ninahitajika hapa Polisi nami nilifika na kisha kuambiwa ninatuhumiwa kuchochea wananchi kulima bangi na kuchochea wananchi nikiwa bungeni kuwa wavamie mgodi wa Acacia North Mara.

“Mimi napinga tuhuma hizo ninazoshitakiwa nazo kwani maswala ya bungeni huishia bungeni sasa hapa uraiani yanafikaje? Nimekwama hapa mahabusu tangu asubuhi hadi sasa sijapatiwa dhamana mbali na ndugu zangu hao mnaowaona hapo nje waliofika kunidhamini, dhamana ni haki ya mshitakiwa kwa tuhuma kama hizo ambazo hazina ukweli,” alisema Heche akiwa chini ya ulinzi wa Polisi.

Kwa upande wake, Matiko alihojiwa na kisha kupewa dhamana na kutakiwa kufika leo kituoni hapo. Aidha, jana katika kituo hicho, Matiko baada ya kuachiwa pamoja na baadhi ya viongozi na wanachama wa Chadema, walikuwa wakishughulikia dhamana ya Heche.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Responsive Ads Here