JPM: WATANZANIA NIOMBEENI - KATUMA BLOG tz.

HABARI ZA HIVI PUNDE

KWA HABARI ZA UHAKIKA NA KUAMINIKA


Post Top Ad

Responsive Ads Here

Monday, November 9, 2015

JPM: WATANZANIA NIOMBEENI

RAIS Dk John Magufuli amewataka Watanzania wa dini zote na viongozi wa dini kutoka madhehebu mbalimbali, kuendelea kumuombea ili atekeleze ahadi alizozitoa pamoja na kuinua maisha ya Watanzania.

Dk Magufuli aliyasema hayo kwenye Ibada ya Mavuno iliyofanyika katika Kanisa Katoliki la Mtakatifu Petro lililopo Oysterbay jijini Dar es Salaam jana. Aliwashukuru pia wananchi wote waliomuombea na kufanikisha kuchaguliwa kuwa Rais wa Tanzania wa Serikali ya Awamu ya Tano.

Katika siku ya nne akiwa ofisini na Jumapili yake ya kwanza tangu alivyoapishwa kuwa Rais wa Tanzania, aliwasili kanisani hapo saa 12.50 asubuhi akiambatana na mkewe, Janet. “Natoa shukurani kwa Watanzania wote wenye imani za kidini tofauti kwa sala zao.

Nawaomba waendelee kuniombea ili niweze kutekeleza ahadi nilizotoa, lakini pia niinue maisha ya Watanzania,” alisema Dk Magufuli alipopewa nafasi ya kuzungumza. Alisema anaamini kuwa ana deni kubwa kwa Watanzania hivyo aliahidi kufanya kazi kwa bidii na kuboresha utoaji wa huduma kama njia ya kutimiza wajibu wake kwao.

“Sala zenu ni muhimu sana, zitaniwezesha kufikisha nchi yetu katika hatua nyingine bora zaidi,” alisisitiza. Awali, wakati akimkaribisha kanisani hapo, Mwenyekiti wa Parokia ya Mtakatifu Petro, Dk Adelhelm Meru, alisema kwa kawaida Watanzania na Waafrika kwa ujumla wana utamaduni wa kutoa shukurani pale wanapopata mafanikio.

“Huu ni utamaduni tuliorithi tangu vizazi na vizazi ndio maana nakuomba leo mheshimiwa Rais, uje usalimie katika mkutano huu,” alisema Dk Meru ambaye pia ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii. Dk Magufuli ni mmoja wa waumini katika parokia hiyo ya Mtakatifu Petro kama ilivyokuwa kwa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.

Ibada hiyo pia ilihudhuriwa na waumini wengi ambao pia ni viongozi kama vile Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Jaji mstaafu Damian Lubuva, Jaji mstaafu Thomas Mihayo na aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Italia, Profesa Costa Mahalu.

Tangu aingie Ikulu Alhamisi iliyopita, Dk Magufuli ameonesha kuwa ni Rais anayechapa kazi ambapo pamoja na kufanya kampeni nchi nzima kwa muda wa miezi miwili, ameendelea kuwajibika ofisini hapo bila kupumzika. Alhamisi iliyopita, alimuapisha Mwanasheria Mkuu George Masaju aliyemteua muda mfupi tu baada ya kuapishwa.

Lakini pia siku moja tu baada ya kuingia Ikulu, Rais alifanya ziara ya kushtukiza katika Wizara ya Fedha ambako aliagiza maofisa wa wizara hiyo kuhakikisha wanaongeza kasi ya ukusanyaji mapato kupitia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), hususani kwa wafanyabiashara wakubwa bila kuogopa.

Katika siku yake ya tatu ofisini, Dk Magufuli pia alikutana na Makatibu Wakuu, Manaibu Katibu Wakuu pamoja na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Profesa Benno Ndulu na Kamishna Mkuu wa TRA, Rished Bade.

Katika mkutano huo, aliagiza kuwa hakuna ofisa yeyote wa Serikali atakayeruhusiwa kusafiri nje ya nchi na badala yake, maofisa wote waelekeze nguvu zao katika maeneo mbalimbali nchini.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Responsive Ads Here