CCM KUENDELEA KUTEGEMEA MATAJIRI NI KUJIDHALILISHA - JK - KATUMA BLOG tz.

HABARI ZA HIVI PUNDE

KWA HABARI ZA UHAKIKA NA KUAMINIKA


Post Top Ad

Responsive Ads Here

Friday, July 10, 2015

CCM KUENDELEA KUTEGEMEA MATAJIRI NI KUJIDHALILISHA - JK

MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM),  Jakaya Kikwete amesema kitendo cha kutumia matajiri kama vyanzo vya mapato,  kunadhalilisha  chama hicho na haiwezi kuendelea kuvumiliwa.

Alisema hayo jana wakati wa uzinduzi wa Kituo cha Mikutano cha CCM mjini Dodoma.

Alionesha  kukerwa na uwajibikaji wa viongozi wa wilaya na mikoa wa chama hicho katika kubuni mapato ya chama hicho hivyo kutumia matajiri kama vyanzo vya mapato.
 

Tunavyo viwanja vingi sana lakini hatuvitumii kuvigeuza mtaji wa kupata kipato. Vipo viwanja vingine viongozi wanagawana; wanajenga nyumba zao badala ya kujenga miradi ya chama. Hili tunalisema tunarudia lakini viongozi wetu hawasikii wao wanakimbilia kwa matajiri kuomba, tunajidhalilisha; lini tutazinduka, alisema.


Katika uzinduzi huo uliohudhuriwa na viongozi wa juu wa chama, Kikwete aliagiza viongozi wa chama hicho kubuni mikakati ya kuhuisha rasilimali za chama hicho ili kukiongezea mapato.

Alisema kituo  kinazinduliwa katika wakati muafaka ambao vikao vya juu vya chama hicho vinafanyika na kwamba kituo hicho kitaandika historia kwa wajumbe kukitumia ili kupata uongozi mpya ndani ya chama hicho.

Miongoni mwa waliohudhuria hafla hiyo ya uzinduzi ni pamoja na  Makamu wa Rais, Dk Mohamed Gharib- Bilal, Makamu Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein, Katibu Mkuu Abdulrahman Kinana, Mwenyekiti wa Bodi ya Udhamini ya CCM, Anna Abdallah na wajumbe wa Kamati Kuu (CC) ya chama hicho.

Alisema  ujenzi wa jengo hilo lililojengwa na Kampuni ya CRJE ya China kwa siku 212, umewafumbua macho wanaCCM kwani sasa watatambua kuwa inawezekana kutumia rasilimali mfu za chama hicho katika kuingizia mapato.
Muonekano wa ukumbi huo mpya


Alisema kwa miaka mingi CCM imekuwa katika hali ngumu ya mapato huku ikiwa na rasilimali nyingi mfu. Alisema  ni lazima sasa rasilimali hizo zikiwemo utajiri mkubwa wa viwanja na maeneo, zigeuzwe kuwa hai na kukiongezea mapato chama hicho.

Alisema alipohutubia Mkutano Mkuu mwaka 2012, alieleza azma yake ya kuhakikisha chama kinajenga jengo jipya na la kisasai kumaliza kero ya kutumia ukumbi wa kukodi wa Kizota.

Kwa mujibu wa Kikwete, ukumbi huo ni ghala linalotumika kuhifadhia mahindi na hivyo  huondolewa ili mikutano ya CCM kufanyika, hatua ambayo hugharimu chama kati ya Sh milioni 800 na Sh bilioni moja.

Alisema pamoja na kupitishwa kwa sera ya kujitegemea,  bado viongozi wa chama hicho wanashindwa kutekeleza sera hiyo kwa vitendo; badala yake wanaendelea kukumbatia rasilimali mfu za chama hicho bila kubuni namna ya kuzihuisha na kuingiza fedha nyingi kwa chama.

Alisema ili kuhakikisha sera ya kujitegemea inatekelezwa kikamilifu, kuna ulazima sasa kwa CCM kuajiri Mkaguzi atakayepita kila wilaya na mkoa kuhakiki vitega uchumi vya chama hicho kwa kuvitembelea na si kupewa taarifa ofisini.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Responsive Ads Here