NYOMOLELO:WANANCHI WA MUFINDI MSITEGEMEE MAENDELEO KULETWA NA CCM - KATUMA BLOG tz.

HABARI ZA HIVI PUNDE

KWA HABARI ZA UHAKIKA NA KUAMINIKA


Post Top Ad

Responsive Ads Here

Thursday, August 27, 2015

NYOMOLELO:WANANCHI WA MUFINDI MSITEGEMEE MAENDELEO KULETWA NA CCM




 Na Mwandishi wetu

MGOMBEA Ubunge wa Jimbo la Mufindi Kusini Mkoani Iringa kwa tiketi ya Chama Cha ACT-Wazalendo Salim Nyomolelo amesema wananchi wa jimbo hilo wasitegemee maendeleo kuletwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) kutokana na chama hicho kuwa chanzo kikuu cha rushwa na ufisadi.

Anasema sababu kubwa ya wananchi kuendelea kukabiliwa na changamoto nyingi za kiuchumi na huduma za jamii ni kutokana na ufisadi ambao upo ndani ya jimbo hilo na njia pekee ni kuitoa CCM katika uchaguzi kwa njia ya sanduku la kura Octoba 25 mwaka huu.

Anasema kuwa jimbo la Mufindi kusini lina fursa nyingi za kiuchumi lakini zinawanufaisha watu wachache kutokana na mianya mingi ya ufisadi inayofanywa na viongozi huku wawakilishi wa wananchi ambao ni madiwani wabunge wakikaa kimya na kuacha wananchi wakiendelea kuteseka.

“Halmashauri ya wilaya ya Mufindi kumekuwa na ufisadi mkubwa ambao unawashirikisha viongozi wa kisiasa wa CCM kwa kufuja fedha ambazo zinatakiwa kutekeleza miradi ya wananchi na ndio sababu kubwa ya madiwani na Mbunge kushindwa kuzungumzia kuhusu ufisadi kwa kuwa nao ni wahusika wakuu,” alisema.

Nyomolelo anasema licha ya viongozi mbalimbali katika Halmashauri hiyo kuhusika na ufisadi lakini wamekuwa wakihamishwa vituo vya kazi kutokana na kuwa na mtandao mkubwa kuanzia ngazi ya wilaya, Wizara ya Tamisemi pamoja na Hazina.

Anasema kuwa ripoti ya kamati ya kudumu ya Bunge ya hesabu za serikali za mitaa ya mwaka 2012/2013 iliyokuwa ikiongozwa na Mohamed Mobarock (CCM) ilionesha jumla ya Halmashauri 70 kati ya 134 zilikuwa na ubadhilifu ikiwamo Mufindi ambapo ubadhilifu huo ulishirikishwa na viongozi wasiowaaminifu katika wizara ya Tamisemi na Hazina.

Aliongeza kuwa CCM iliongoza jimbo hilo tangu Uhuru lakini imeshindwa kukidhi matakwa ya wananchi licha ya halmashauri hiyo kuwa ya pili katika kuchangia pato la taifa lakini wananchi hawanufaiki na mapato hayo kutokana na huduma za jamii kuendelea kuwa mbovu hivyo wananchi wasitegemee jipya kutoka CCM zaidi ya kuendeleza ufisadi.

Hata hivyo, Nyomolelo alisema njia pekee ya kuwawajibisha viongozi wa aina hiyo dhidi ya ufisadi ni kukichagua chama cha ACT-Wazalendo ambao kinaongozwa na mtetezi wa wanyonge katika nchi hii Zitto Kabwe ambapo pia chama hicho pia kinaongozwa na misingi na miiko ya viongozi ili kukabiliana na ufisadi uliokithiri hapa nchini.



No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Responsive Ads Here