MO AACHA VILIO, MAJONZI SINGIDA, MWENYEWE AJIVUNIA MAFANIKIO - KATUMA BLOG tz.

HABARI ZA HIVI PUNDE

KWA HABARI ZA UHAKIKA NA KUAMINIKA


Post Top Ad

Responsive Ads Here

Thursday, July 9, 2015

MO AACHA VILIO, MAJONZI SINGIDA, MWENYEWE AJIVUNIA MAFANIKIO

IMG_7558

Na Modewjiblog team, Singida
 
MBUNGE  wa Singida mjini na mfanyabiashara maarufu nchini, Mohammed Dewji,  amesema hatagombea ubunge wa jimbo hilo tena baada ya kulitumikia kwa miaka 10 na kuwezesha maendeleo makubwa katika sekta za elimu na afya.

Mbunge huyo alisema hayo akihutubia maelfu ya wananchi waliokusanyika katika  uwanja wa People's Club wakati wa uwasilishaji wa utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi ya mwaka 2005/ 2010 na 2010/ 2015 kwenye mkutano mkuu wa jimbo.  Katika utekelezaji huo ametumia Sh bilioni 5.

Miradi hiyo ni pamoja na kusaidia kuongeza shule za sekondari kutoka mbili hadi 15, kuwapo kwa vituo vya afya na kupeleka shule watu wenye mazingira magumu 15,000.

Kauli yake hiyo iliyowaliza baadhi ya wapiga kura wake aliitoa huku akisema  amechukua uamuzi huo ili kutoa fursa kwa makada wengine wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kugombea jimbo hilo.

Tamko hilo la Dewji lilipokelewa kwa masikitiko makubwa kwani hata alipofikia nukta ya tamko hilo na kutoa salamu  ya Chama hicho;  yaani “CCM Oyee”  hakuna aliyeitikia inavyostahili zaidi ya kusema “Hatutakiiii”.

Alisema kuwa alipoanza safari yake ya kisiasa miaka 10 iliyopita, lengo lake kuu lilikuwa kuleta maendeleo kwa wananchi wa jimbo hilo. “Pamoja na uamuzi wangu wa kutokugombea, lengo langu linabaki pale pale”, alisema huku umati ukimwangalia kwa mshangao mkubwa.

Alisema ametekeleza majukumu yake ya kusukuma maendeleo katika jimbo lake la uchaguzi kwa ushirikiano mkubwa na kufanikisha vipaumbele vya  wakati huo ikiwamo elimu na Afya.

Alisema kwamba  kujiondoa kwake katika siasa za jimboni kunatokana na majukumu ya biashara zake kuwa makubwa pamoja  na kutaka kuwa karibu na familia yake baada ya miaka 10 ya kuwatumikia wananchi wa Singida.

"Ukichukulia kuongezeka kwa-mvi kichwani, ukilinganisha wakati wa awamo ya kwanza, nafikiri ni busara sasa kutimiza majukumu haya ya familia ambayo niliyabania nafasi yake kwa kipindi cha miaka 10.

"Pia siyo siri kwamba majukumu ya biashara zangu yamebadilika katika kipindi cha miaka ya hivi karibuni. ukuaji wa biashara zangu umeambatana na kuongezeka kwa majukumu, hususan mahitaji ya muda zaidi," alisema.

Akizungumzia sekta ya afya alisema wananchi wa Singida walifanikiwa kukabiliana vilivyo na ugonjwa hatari wa malaria kwa kugawa vyandarua zaidi ya vyandarua 6,000 kwa mama wajawazito na watoto chini ya miaka 5. 

"Kwa kusambaza vyandarua hivi, tulifanyikiwa kupunguza vifo vya watoto chini ya miaka 5 kwa asilimia hamsini" alisema akishangiliwa.

Aidha alishirikiana na mamlaka husika kupambana na ugonjwa sugu wa mtoto wa jicho kwa kupeleka madaktari bingwa na kufanya kambi kwenye hospital  ya mkoa, waliotoa huduma ya upasuaji wa jicho na kutoa miwani kwa zaidi ya wananchi 1,000.

"Tulifanikiwa kujenga wodi ya macho, ndani ya hospitali yetu ya mkoa.  Tulifanikiwa kuchangia ujenzi, wa zahanati za Mungumaji, na Manga ambazo zimekamilika! na zahanati ya kijiji cha Ititi ambao bado ujenzi unaendelea," alisema.

Pamoja na ujenzi huo pia alielezea kusaidia baiskeli kwa walemavu na kufunga nishati ya umeme jua, pamoja na majokofu ya kutunzia dawa, kwenye zahanati za Manga na Unyambwa!

Akifafanua zaidi katika sekta ya elimu alisema kwamba walijenga vyumba vya madarasa, kuweka matangi ya maji ya kuvunia maji ya mvua, vyoo, na kusambaza madawati katika shule mbali mbali za msingi na sekondari  jimboni Singida mjini.

Aidha alichangia vitabu zaidi 1000, vya masomo ya sayansi na sanaa, kwa shule za serikali ndani ya manispaa ya Singida.

Akizungumzia sekta ya maji walifanikiwa kuchimba visima viwili kwenye mtandao wa Suwasa na vingine 45 ndani ya baadhi ya vitongoji vyetu vya manispaa ya Singida.

Aidha alisema alifanikiwa kusukuma mradi wa visima 10, unaofadhiliwa na benki ya dunia, akisisitiza kuwa wakati akiingia mwaka 2005 upatikanaji wa maji safi na salama ulikua asilimia 23 na sasa upatikanaji wa maji umefikia asilimia 81.

Pia alisema amefanikiwa kuisukuma serikali, kujenga barabara za kiwango, cha changarawe ndani ya manispaa na kufanya manispaa kuwe na barabara zinazopitika kwa kipindi chote!

Akiwashukuru wananchi wa Singida alisema kwamba: "kuwatumikia ninyi imekuwa ni tunu kubwa sana niliyobarikiwa katika kipindi hiki cha miaka 10, na najisikia kuwa nimependelewa kwa kujifunza mambo mengi yanayohusu Singida na uongozi bora, na hususan mapungufu yake, ikiwemo mimi mwenyewe."

Alisema dhamira yake kwa wananchi haitokani na nafasi yangu kama mbunge ama mwanasiasa, akisisitiza kuwa dhamira yake ya uzaliwa inayotokana na mapenzi aliyonayo kwao na imani aliyonayo juu ya uwezo wa kuijenga Singida.

Mkutano huo mkubwa wa aina yake ulipambwa na mwanamuziki nyota wa kizazi kipya nchini, Nasib Abdul maarufu kama “Diamond Platinum”.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Responsive Ads Here