Huwa inatokea mwili wako
kutoa harufu ambayo inakera kwa wengine au kwako mwenyewe kuivuta puani. Harufu
hii inafanya hata nguo ulizovaa zitoe harufu, inaharibu uhusiano na kufanya
watu wengine wakuepuke.
Sikiliza hii nukuu:
"Wakati mwingine, mtu mwenye tatizo linalokera, si yeye anayekereka,
badala yake wanaokereka ni wale watu anaoishi nao ama kufanya nao kazi."
Mwili wako unapotoa harufu
isiyopendeza, utawaudhi watu kila unapokwenda, iwe kwenye basi, kwenye maduka
yaliyojazana watu au hata kwenye sehemu za vinywaji kama vile baa. Na hasa
utamuudhi kabisa mpenzi wako kama si mke wako.
Mara nyingi harufu ya mwili,
uchunguzi unaonesha, inawatoka sana wanaume kuliko wanawake (tutaangalia hili
baadaye).
Kama harufu unagundua kwamba
inatoka kwenye mwili wako, wewe mwenyewe utapatwa na mteru (panic) kidogo. Kama
inatoka kwa mtu mwingine, atakukera lakini wewe utajisikia hauna balaa. Mara
nyingi kama inatoka kwa mtu unayemheshimu, kiustaraabu utaogopa kumwambia
lakini unaweza kuwaambia wengine kuhusu huyo mtu.
Harufu inatokana na nini?
Harufu hii mara nyingi
inatokana na jasho. Ni vyema ieleweke kwamba kiuhalisia jasho halina harufu
kabisa. Kinacholeta harufu ni bakteria ambao huishi kwenye ngozi na ndio
wanaobadilisha jasho hili na kuwa harufu isiyopendeza.
Mtu huzalisha jasho la aina
mbili, apocrine na eccrine.
Jasho aina ya eccrine hufanya
kazi ya kurekebisha ama kupunguza joto mwilini, na hutokea wakati mtu
anapofanya mazoezi, kazi ngumu ama kunapokuwa na joto jingi kama ilivyo kwa
jiji kama Dar es Salaam sasa.
Apocrine ni jasho maalumu
analotoa mtu katika baadhi ya maeneo, kama vile katikati ya vidole vya mikono
ama miguu, sehemu za siri hususani katikati ya mapaja au kwenye korodani kwa
wanaume, kwenye makwapa au hata kwenye mfereji uliopo karibu na tundu la haja
kubwa.
Ingawa majasho yote haya
huweza kumletea mtu taabu, lakini jasho hili la apocrine ndilo tishio zaidi kwa
harufu.
Kinachotokea, kama ambavyo
tumeshadokeza hapo juu ni kwamba baadhi ya bakteria wa asili katika mwili hula
jasho la apocrine na wanapokuwa katika harakati za kula jasho hilo huzalisha
kemikali ambazo ndizo hutoa harufu isiyopendeza.
Kuwa na uzito mwingi, kula
chakula kama vile chenye vitunguu zaidi, samaki na viungo vingi husababisha
jasho hili kuongezeka.
Kutoosha ama kuvaa nguo
ambayo ni chafu siku baada ya siku, hufanya jasho kuganda kwenye nguo, hali
ambayo huvutia bakteria wengi zaidi na kusababisha harufu kali zaidi.
Kwa nini wengine miili
hainuki?
Sababu kubwa ya mwili kutoa
harufu, kitu ambacho pia kinaweza kuvutia magonjwa mengine, hususani ya ngozi,
ni mtu kutokuwa msafi. Kuna wale ambao hawafui nguo na hawaogi kadri inavyostahili.
Kwa mantiki hiyo usafi
hauishii katika kuoga tu asubuhi na jioni, bali pia kufua nguo zako kila baada
ya kuzivaa mara moja.
Pia nguo za pamba zinaaminika
kuwa nzuri zaidi ya zingine kwa sababu zinaweza kumeza harufu mbaya kirahisi na
kupunguza joto.
Vile vile watu wanapishana
kuhusu idadi ya bakteria walio nao katika miili yao. Kuna watu wana bakteria
wengi wanaokula jasho na kuzalisha kemikali zinazonuka kuliko watu wengine.
Hili ni suala la maumbile. Hata hivyo, wote hawa wanatakiwa kuimarisha usafi.
Sababu nyingine ya kupisha
harufu mwili ni mambo yanayosababisha jasho. Kuna watu wanafanya kazi zenye
kutoa jasho zaidi kuliko wengine ama wanafanya kazi kwenye mazingira ya joto
kuliko wengine na pia wengine hufanya mazoezi ya kutoa jasho na wengine
hawafanyi.
Watu wengine mijini, wanakuwa
na muda mwingi wa kufanya kazi kuliko ule wa kupumzika kwa hiyo unakuta
hawapati ama wanakuwa wavivu kuangalia suala la usafi wa miili yao au nguo zao.
Kitu kingine kinachoudhi ni
muguu inayonuka, na hasa mwenye kunuka miguu anapovua soksi. Hili ni tatizo
wanaloita la kawaida la mwili ingawa pia harufu kutoka mtu mmoja hadi mwingine
hupishana pia. Tatizo hili hukabili theluthi moja tu ya wanawake lakini karibu
asilimia 50 ya wanaume hunuka miguu yao na wakivua soksi na viatu vyao, mh...
ni hatari!
Kutokana na mwili kuwa na
mamilioni ya tezi zinazozalisha jasho, miguu yetu hutoa hadi lita nne na nusu
ya jasho kila wiki!
Tatizo la kunuka miguu
linaweza kudhibitiwa kwa njia za kawaida tu na wala si matibabu, labda kama mtu
anaugua fangasi. Kubwa kuhusu kuondokana na tatizo hili ni kuosha na kukausha
vidole vya miguuni, hususani nyufa zinazotenganisha kidole kimoja na chenziye na kuvaa viatu au soksi inazopitisha hewa.
Lakini pamoja na hayo, kuna
vitu vingi vinatengenezwa viwandani katika kupunguza harufu ya miguuni. Tatizo
linapoonesha kuwa kuna bakteria wengi wanaozalisha kemikali katika eneo hilo
ambazo ndizo hunuka, mtu anashauriwa kumuona daktari. Anaweza kupewa dawa za
krimu, antibiotics na kadhalika.
Wanaume na wanawake
Tafiti zinaonesha wanaume
wengi huwa na harufu mwilini isiyopendeza kulinganisha na wanawake. Sababu
kubwa ni wanaume kujishughulisha na mambo mengi ya kutoa jasho kulinganisha na
wanawake.
Pia tafiti zinaonesha kwamba
wanaume si watu wa kujishuku sana kama wanatoa harufu kulinganisha na wanawake.
Kadhalika maumbile ya
wanawake huwalazimisha kuoga mara kwa mara kulinganisha na wanaume.
Tafiti pia zinaonesha kwamba
wanawake hupendelea sana kutumia manukato ya kuondoa harufu ya mwili kuliko
wanaume.
Mambo muhimu ya kufanya
Tumeona kwamba kimsingi jasho
la mtu halinuki lakini husababisha harufu linapoliwa na bakteria, kwa hiyo njia
kubwa ya kufanya mwili usinuke ni ama kuondokana na jasho, kuliondoa haraka
mwilini ama kuua bakteria walioko kwenye mwili.
Kwa vile mazingira
yanatulazimisha kutoka jasho, ni muhimu kuliondoa jasho kila mara kwenye miili
yetu, na hivyo tunapaswa kuzingatia usafi.
Maeneo muhimu ambayo
yanasisitizwa kufanyiwa usafi ili kuondoa jasho na bakteria ni yale ya kwenye
kwapa, vidole vya miguu ama maeneo ya sehemu za siri.
Katika kwapa, pia inashauriwa
mtu kunyoa nywele za eneo hilo mara kwa mara kwa sababu hazina lolote zaidi ya
kufuga bakteria na kuwapa mahala pazuri pa kuzaliana pamoja na kukaribisha jasho zaidi.
Pili, ni muhimu sana kufua
nguo zako vizuri kabisa kwa sabuni, hasa zile ambazo zinavaliwa katika maeneo
yenye jasho jingi kama vile soksi, nguo za ndani na fulana. Usivae nguo uliovaa
jana hata kama unadhani bado inafaa kwa sababu lazima nguo hiyo ina kijiharufu
kilichotokana na jasho la jana.
Tatu, inatakiwa mtu aoge mara mbili au zaidi kwa siku, hususan katika
jiji lenye joto kama Dar es Salaam. Pia inatakiwa kujali sabuni zinazoaminika
kuua bakteria kwenye mwili. Hizi husaidia kupunguza bakteria ambao huozesha
jasho haraka.
Nne, ni vizuri kutumia
manukato ya kawaida kwa sababu yanakufanya unukie vyema na watu kupenda kuwa
nawe karibu. Lakini jihadhari kama manukato hayo yanawakera wengine mnaokuwa
nao maofisini. Wengine wana mzio na manukato.
Tano, jikaushe vyema kwa
taulo kila unapotoka bafuni na mwisho epuka kula vyakula vilivyoungwa sana ama
vinavyotoa haufu kali.
Kumuona daktari
Kuna wakati jasho linalomtoka
mtu ni jingi mno na si la kawaida. Hapo mtu anaweza kumuona daktari ili
kupunguza jasho hilo lisilo la kawaida. Mtu wa aina hii pia anaweza kufanyiwa
upasuaji ili kuondolewa idadi ya tezi zinazozalisha jasho jingi mwili mwake.
Kama mtu ana magonjwa ya
ngozi katika maeneo yenye jasho jingi, yaani makwapani, vidoleni na sehemu za
siri, pia anatakiwa kumuona daktari haraka.
Kumbuka pia kwamba harufu
fulani inaweza kuonesha kuwa mhusika anasumbuliwa na ugonjwa fulani. Kwa mfano,
harufu kama ya bia inaonesha kuwa mtu huyo ana fangasi wengi na hawa mara
nyingi hukaa ukeni.
Harufu kama ya polish inaweza
kuonesha kuwa mhusika ana ugonjwa wa kisukari na harufu kama ya ammonia,
inaweza kuonesha kuwa mhusika ana tatizo la ini.
No comments:
Post a Comment