'MAWAZIRI PUNGUZENI SAFARI' - KATUMA BLOG tz.

HABARI ZA HIVI PUNDE

KWA HABARI ZA UHAKIKA NA KUAMINIKA


Post Top Ad

Responsive Ads Here

Friday, June 19, 2015

'MAWAZIRI PUNGUZENI SAFARI'



WATENDAJI serikalini pamoja na mawaziri wametakiwa  kupunguza safari za nje ya nchi, badala yake waende vijijini kusikiliza na kutatua matatizo ya wananchi.

Katibu wa Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Nape
 Nnauye alitoa tamko hilo juzi mjini Masumbwe, wilayani Mbogwe wakati akihutubia mkutano wa hadhara.  

Nape ambaye pamoja na Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana  wako mkoani Geita kuangalia utekelezaji na uhai wa chama, alisema ambaye hatasikia agizo hilo, atashughulikiwa mambo yaende sawa katika chama.  

Akisisitiza viongozi hao kutoka  maofisini kwenda kwa wananchi, alisema viongozi wakiacha kukaa Dodoma, na Dar es Salaam wakaenda vijijini, maendeleo ya wananchi yatakwenda haraka.

 
“Nataka nitoe mwito kwa watendaji wa serikali kuanzia huko juu, tusianzie huku chini, Mawaziri watoke maofisini wapunguze safari za kwenda Ulaya, waje Mbogwe washughulikie matatizo ya watu,” alisema Nape. 

Alisisitiza, “Kama sisi tuliopewa dhamana na wananchi tunazunguka, basi tunawataka na Mawaziri wazunguke washughulikie matatizo ya watu.” 

Alisema yako matatizo mengi ya wananchi waliyobaini kupitia ziara hizo za Katibu Mkuu Kinana ambazo kama Mawaziri watakwenda kuyasikiliza, ufumbuzi wake utapatikana mara moja.  
 
Alisema, “Na sasa kwa kuwa masikio hayavuki kichwa, naamini watatusikia, asiyetusikia tutashughulika naye ili mambo yetu yaende sawasawa.” 

Kwa mujibu wa Nape, tangu waanze ziara kuanzia mkoani Kagera na sasa  Geita, kila wanakopita,  yako mambo kadhaa ambayo yanakwenda taratibu kutokana na wenye dhamana ya utatuzi kutozuru mikoani.  

Alisisitiza lengo la  ziara ya Kinana  ni kuongeza kasi ya kutatua matatizo ya wananchi. “Watoke maofisi waje washughulikie matatizo ya watu,” alisema Nape na kuongeza kwamba  chama kikiendelea kushughulikia matatizo ya watu, Watanzania wataendelea kukiamini.  
 
Hata hivyo, alisema wameendelea kushughulikia  matatizo ya watu, hali ambayo inaifanya CCM kuwa madarakani.  Wakati huo huo, Nape aliendelea kuhadharisha juu ya watu wenye mwelekeo wa kuvunja amani ya nchi na kuwataka vijana kuepuka kuingia mtego huo.
 
Katika ziara ya Katibu Mkuu wa CCM mkoani Kagera na Geita, amebaini kero mbalimbali zinazokabili wananchi  miongoni mwake ikiwa ni  migogoro ya ardhi, matatizo ya maji, utitiri wa vizuizi barabarani, bei ya chini ya mazao hususani kahawa na pamba na kodi nyingi.  

Katika mikutano mbalimbali ya hadhara aliyoifanya  kwenye mikoa hiyo,  Kinana ameahidi kukutana na mawaziri wenye dhamana kwa ajili ya kutafuta ufumbuzi wa matatizo hayo yanayokwamisha maendeleo ya wananchi.  

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Responsive Ads Here